Home » , , , , , » BILALI REHANI WAIKELA...

BILALI REHANI WAIKELA...

Written By mahamoud on Friday, December 27, 2013 | 10:26 AM





Bilali Rehani Waikela akitoka Mahakama ya Kisutu Dar es Salaam alipokuja kutoa ushahidi kesi ya Sheikh Ponda




Naweka hapa chini yale ambayo niliandika katika kitabu changu, ''Maisha na Nyakati za Abdulwahid Sykes...'' kuhusu Mzee Bilal Rehani Waikela:

''Napenda kutoa shukrani maalum kwa Bilal Rehani Waikela, muungwana wa Kimanyema na Muislamu wa kweli. Waikela akiwa na umri wa miaka ishirini na tano mwaka 1955, alikuwa mmoja wa waasisi wa TANU mjini Tabora. Waikela alinieleza jinsi Waislam kwa umoja wao walivyomuunga mkono Julius Nyerere na harakati za uhuru. Vilevile vilevile alinieleza kwa muhtasari siku zake kizuizini pamoja na babu yangu katika gereza la Uyui, Tabora kwa kile kilichoitwa kosa la ëkuchanganya dini na siasa.í  Nina deni kubwa kwake kwa kunipa picha za wakati ule na nyaraka zake binafsi juu ya ëmgogoroí wa EAMWS uliozushwa mara baada ya uhuru. Natoa shukrani kwa Waikela kwa kunitia hima na kunipa moyo kuandika kitabu hiki ili nieleze kuhusu dhulma waliofanyiwa Waislam na utawala wa Nyerere. Waikela tofauti na watu wengine waliozungumza na mimi aliniruhusu pia kumnukuu kwa jina bila ya woga wowote.  Alifurahi kuona kwamba historia ya kweli ilikuwa inaandikwa na habari alizonieleza zitakuja kutumika katika kuhifadhi historia ya nchi yetu kwa faida ya vizazi vijavyo. Vilevilevilevile Waikela alinikutanisha na wazalendo wengine kama Mohamed Mangiringi, marehemu Ramadhani Singo na wengineo ambao nilizungumzanao kwa kirefu.

Mwaka 1955 Bibi Titi Mohamed na Julius Nyerere waliitika mwaliko na kuja Tabora. Mkutano ulifanyika katika ile kilabu ya kandanda. Waliohudhuria mkutano ule walikuwa Germano Pacha, Juma Mrisho, Shaaban Mohamed Silabu, Bilali Rehani Waikela, Mohamed Mataka wakati ule akiwa muadhin wa Masjid Nur - msikiti wa Wamanyema pale Tabora, Hassan Mohamed Ikunji, Ramadhani Mussa Wajaku, Swedi Mambosasa, Said Ali Kiruwi na Hamis Khalfan. Uongozi wa kilabu ulimwambia Nyerere na Bibi Titi  kuwa kilabu hiyo ya kandanda ilikuwa ikitaka udugu na TANU ili ifanye kampeni ya kuipatia TANU wanachama wengi. Uongozi huo wa TANU kutoka makao makuu Dar es Salaam uliambiwa kuwa maadam kilabu hiyo ilikuwa ikipendwa na kuungwa mkono na watu wa Tabora na ilikuwa maarufu sana, sifa hizo zingeweza kutumiwa kwa manufaa ya TANU. Vilevile Nyerere alifahamishwa kuwa  kilabu hiyo ingependa kuvijumuisha vyama vitatu vya lelemama na vikundi vya taarabu, Nujum ul Azhar, Waridatil Hubb na Egyptian Club. Nyerere na Titi waliyakubali mapendekezo haya na usiku ule akifuatana na uongozi wa kilabu Nyerere alizungumza na kikundi cha watu waliyokusanyika nje ya nyumba ya kilabu juu ya hali ya Tanganyika katika siku zijazo. Nyerere alikuwa amerudi Tabora ambapo alianza siasa kiasi cha miaka minane nyuma. Jambo muhimu katika kipindi hiki pale Tabora ni kuwa wasomi wa Makerere waliokuwa St. Maryís School hawakuwapo katika harakati hizi na katika mikakati iliyokuwa ikipangwa.

Bibi mmoja wa Kiganda, Nyange bint Chande, mwanachama wa moja ya vikundi vya lelemama mjini Tabora alijitolea nyumba yake kama ofisi ya kwanza ya TANU katika Jimbo la Magharibi. Uchaguzi ulifanyika na Shaabani Marijani alichaguliwa Mwenyekiti wa Wilaya na Idd Said Ludete Katibu wa TANU. Bilali Waikela akawa mjumbe wa kamati. Kadi za kwanza za uanachama wa TANU ziliuzwa ndani ya soko la Tabora  na Amani Idd na Pacha, Katibu wa Jimbo wa TANU. Pacha alikuwa na lingo la kuni pale sokoni kama biashara yake. Baadae Amani Idd alisaidiwa kazi hiyo ya kuuza kadi za TANU na Dharura bint Abdulrahman.

Makao makuu ya TANU yaliamua kumtuma Peter Mhando, (mdogo wake Stephen Mhando) kwenda Tabora kufanya uchunguzi na kuandika taarifa ambayo ingetoa msingi wa ufumbuzi wa kudumu kuhusu matatizo yanayoisibu TANU pale Tabora. Wakati ule Peter Mhando alikuwa kijana wa kiasi cha miaka ishirini hivi aliifanya kazi ile na vijana wengine kama Bilal Waikela, Ramadhani Abdallah Singo, Abdallah Saidi Kassongo na vijana wengineo. Vijana hawa walikamilisha taarifa na kuituma makao makuu. Hii ilikuwa ndiyo kazi ya mwisho ya Mhando kuifanyia TANU kwani alifariki kwa ugonjwa wa kisukari mara tu baada ya kutayarisha na kutuma taarifa yake makao makuu ya TANU.

Jaribio la mwanzo la Nyerere kutaka kuivunja EAMWS lilikuwa mwaka 1963. Lakini jaribio hilo halikufanikiwa kwa sababu ya mpango uliopangwa na Mufti Sheikh Hassan bin Amir na kutekelezwa na Bilali Rehani Waikela, katibu wa EAMWS Tabora. Mwaka huu wa 1963 EAMWS ilifanya mkutano wake katika ukumbi wa Shule ya wasichana ya Aga Khan. Wajumbe wa mkutano huo walipowasili mjini Dar es Salaam walikuta uvumi kuwa wajumbe wa mkutano wa EAMWS watakamatwa na kuwekwa kizuizini. Chanzo cha uvumi huu hakikufahamika lakini haikuwa vigumu kuhisi. Baada ya kuvunjwa kwa Baraza la Wazee wa TANU mwaka ule ilikuwa wazi kuwa Nyerere alikuwa amewatupa mkono washirika wake wa zamani na sasa alikuwa akitafuta wapya ili kujenga upya msingi wake wa siasa. Kutokana na mambo yalivyokuwa yakienda ilikuwa ni dhahiri washirika wake wapya hawatakuwa Waislam.

Katibu wa EAMWS Tabora, Waikela alipowasili Dar es Salaam kuhudhuria mkutano aliitwa na Sheikh Hassan bin Amir. Mufti Sheikh Hassan bin Amir mbele ya Mzee Ali Comorian, alimfahamisha Waikela kuwa kulikuwa na njama zilizokuwa zikipikwa na Nyerere kumuungamiza yeye na Tewa Said Tewa ili kuvunja EAMWS ipatikane nafasi ya kuanzishwa jumuiya ya Kiislam ya Watanganyika itakayokuwa chini ya wanafiki. Sheikh Hassan bin Amir alimwambia Waikela kuwa harakati za uhuru zilikuwa zinatekwa nyara na Wakristo kwa manufaa ya makanisa yao. Sheikh Hassan alimfahamisha Waikela kuwa ni lazima yeye afanye kila linalowezekana ili njama za Nyerere zishindwe. Waikela alimuuliza Sheikh Hassan bin Amir kwa nini amechaguliwa yeye kufanya kazi ile. Sheikh Hassan bin Amir alimuambia kuwa yeye ana imani na uwezo wake. Baada ya maneno hayo Sheikh Hassan bin Amir alinyanyua mikono yake juu na kumuombea dua Waikela. Nyerere alikuwa anamfahamu Waikela  kwa kuwa alikuwa muasisi wa TANU na alikuwa ametoa mchango mkubwa katika kupigania uhuru.

Nchi nzima hasa sehemu za Waislam kulikuwa mpango wa serikali wa kuwavunja Waislam nguvu na kuwakatisha tamaa. Waikela, kama ilivyokuwa kwa viongozi wengine wa EAMWS alikuwa anasuguana na Mkuu wa Mkoa wa Jimbo la Magharibi, Richard Wambura. Kulikuwa na ujeuri kwa upande wa serikali walipokuwa wanashugulikia matatizo ya Waislam, mbali na mategemeo ya Waislam waliyokuwanayo kabla ya uhuru. Subira ya Waikela ilifikia kikomo pale Wambura alipowatukana Waislam katika mkutano wa hadhara. Baada ya kuhutubia Wambura, Waikela alipanda jukwaani na akaikumbusha serikali isiwe mwizi wa fadhila kwa kusahau jinsi Waislam walivyojitolea muhanga katika kudai uhuru. Serikali ikachukulia hotuba ya Waikela kama usaliti na yenye kuwashawishi Waislam wasiitii serikali. Ilikuwa katika hali hii Waikela mwanachama shupavu wa TANU alijitoa kwenye chama na akaamua kutumia nguvu zake kuwatumikia Waislam kupitia EAMWS. Ilikuwa wazi kuwa Nyerere alikuwa na habari za msuguano kati ya serikali na Waislam kule Tabora na mtu ambae alikuwa akihusika na msuguano huo.

Siku kabla ya mkutano wa EAMWS, Nyerere aliwaalika wajumbe wa mkutano Government House kwa chakula cha usiku. Hao waalikwa walikuwa wajumbe waliochaguliwa mahsusi. Waikela hakuwa mmoja wa hao waalikwa. Nyerere alichukua nafasi ile kuwashauri wajumbe wale waanzishe jumuiya ya Waislam wa Tanganyika ichukue nafasi ya EAMWS. Wajumbe hawa walipoleta katika mkutano hoja ya kuanzisha jumuiya ya Waislam wa Tanganyika, Waikela alisimama na kuipinga hoja ile. Alizungumza vilevile kuhusu uadui wa serikali kwa Waislam na Uislam. Waikelaalimaliza hotuba yake kwa kutoa changamoto kwa wajumbe wamuite Nyerere kwenye ufunguzi wa  mkutano ili aje awaeleze wajumbe msimamo wake kuhusu kadhia hii ya chinichini baina ya serikali na Waislam.

Baada ya kushindwa kwa hoja ya kuivunja EAMWS wajumbe wa mkutano ikaonekana kuwa ingekuwa vyema Nyerere aitwe kufunga mkutano ule na asomewe makubaliano yaliyofikiwa. Nyerere alifika kufunga ule mkutano na akakutana uso kwa uso na Waikela, ambae alimsomea maazimio ya mkutano. Waikela alimfahamisha Nyerere kuwa umoja kwa Waislam ni fardh ñ wajibu wa lazima. Ni kwenda kinyume na maamrisho ya Allah kuwagawa watu. Baada ya utangulizi huu Waikela huku akimnyooshea Nyerere kidole alieleza uadui unaoonyeshwa na serikali dhidi ya Waislam. Waikela alimaliza hotuba yake kwa kitisho. Alimwambia Nyerere ikiwa Waislam watamgeuka kupambana na yeye hatakuwa na uwezo wa kuwashinda. Nyerere alitulia tuli pembeni mwa Rais wa Baraza la Tanganyika la EAMWS Tewa Said Tewa akimsikiliza Waikela. Aliposimama kujibu hotuba ya Waikela Nyerere kwa upole alisisitiza msimamo wa serikali wa kutoa haki na usawa kwa raia wake wote. 

Kwa kiasi fulani Nyerere alikuwa amefanikiwa kupunguza joto kati ya Waislam na serikali. Hotuba ya Waikela na ya Nyerere zikapewa umuhimu mkubwa katika radio. Waislam wengi wakajitokeza stesheni ya gari moshi Tabora kuja kumpokea shujaa Waikela. Alipewa heshima ile kwa kuwa na ujasiri wa kuweza kusimama kidete dhidi ya wale waliodhani kuwa wanaweza kuwakalia Waislam vichwani. Nyerere alihisi ameumbuka na hili lilimchoma moyo sana. Kuanzia hapa Nyerere hakumtazama Sheikh Hassan bin Amir kwa jicho jema. Alingoja nafasi yake ili alipize kisasi. Mwaka uliofuata, tarehe 20 Januari, 1964 jeshi liliasi. Nyerere alichukua fursa ile kuwatia kizuizini masheikh walioonekana wanapinga serikali na viongozi wa vyama vya wafanyakazi. Waikela alikuwa mmoja wa wale waliokamatwa na kuwekwa kizuizini. [1]Nyerere kwa wakati ule hakuwa na nguvu ya kumgusa Mufti Sheikh Hassan bin Amir...''

In Sha Allah Itaendelea...



Uongozi wa East African Muslim Welfare Society katika ni Solomon Eliufoo (Waziri wa Elimu) na Tewa Said Tewa (Territorial President EAMWS) kulia kabisa aliyevaa kanzu na kilemba ni Mufti Sheikh Hassan bin Amir.


Share this article :

0 comments:

Post a Comment